WARSAW, Poland
CRISTIANO Ronaldo amekutana na shabiki yake mkubwa, ambaye aliamka baada ya kuwa mahututi kwa muda wa miezi mitatu wakati mshambuliaji huyo wa Real Madrid akipiga ‘hat-trick’ kwenye mchezo wa kufuzu fainali za Kombe la Dunia mwaka 2014, kati ya timu yake ya Taifa ya Ureno dhidi ya Sweden.
David Pawlaczyc alipata majeraha makubwa ya ubongo mwaka 2013, baada ya kugongwa na gari wakati anaendesha baiskeli na kukaa wiki 12 bila kupata nafuu.
Wazazi wake waliamua kumpeleka kwa wataalamu, ambao walishauri mtoto huyo ambaye ni shabiki mkubwa wa Ronaldo asikilizishwe mechi ambayo nyota huyo wa Ureno atakuwa anacheza ili kurudisha kumbukumbu zake.
Akiwa katika hali hiyo ya mahututi, David alivalishwa ‘headphone’ wakati Ureno wakicheza mechi ya mtoano ya kufuzu fainali hizo za Kombe la Dunia zilizofanyika Brazil, kijana huyo aliamka mchambuzi wa mechi hiyo alipokuwa akitangaza bao la tatu la Ronaldo.
Kwa ushindi huo, Ronaldo aliihakikishia nchi yake nafasi ya kutinga fainali hizo za Brazil na
Aprili mwaka 2014, Ronaldo alimwalika Pawlaczyc kwenda kuitembelea Madrid kama mgeni maalumu kuangalia mechi ya Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Borussia Dortmund.
Wiki hii, wakati Real wakikutana na Legia Warsaw kwenye mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya juzi Jumatano usiku, Pawlaczyc akiwa na wazazi wake walitumia saa sita kuendesha gari kwa ajili ya kwenda mjini Warsaw kumuona mchezaji wake anayempenda.
Shabiki huyo alipiga picha akiwa amekumbatiana na nyota huyo na kupata saini za mchezaji huyo.
Lakini shabiki huyo wa Ronaldo alikuwa na bahati mbaya, baada ya klabu ya mchezaji anayempenda kutoka sare ya mabao 3-3 kwenye mechi hiyo.
Mabingwa hao watetezi wa Ligi ya Mabingwa Ulaya walipata bao la kuongoza lililofungwa na Gareth Bale, kabla ya kumtengenezea Karim Benzema bao la pili.
Lakini Legia wakicheza kwenye uwanja wao bila mashabiki, walirudi kipindi cha pili kwa nguvu na kusawazisha mabao yote mawili kupitia nyota wao, Vadis Odjidja-Ofoe na Miroslav Radovic, kabla Thibault Moulin kufunga bao la tatu dakika ya 83.
Ila bahati haikuwa yao, baada ya Mateo Kovacic kuisawazishia Madrid, huku wakionekana kwamba wangeibuka na ushindi.