NA MWANDISHI WETU
TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) imeombwa kuchunguza matumizi ya Sh milioni tano zilizotolewa na Mfuko wa Pensheni wa PPF kwa ajili ya uandaaji wa kongamano la wasanii kwa Chama cha Waigizaji Taifa (TDFAA) Februari, mwaka huu.
Akizungumza na BINGWA, Mjumbe wa Bodi na Mhasibu wa Chama cha Waigizaji Taifa (TDFAA), Lydia Mgaya, alisema toka PPF watoe fedha hizo hakuna kitu kilichofanyika, hali iliyopelekea wanachama kutoka mikoani kuanza kuhoji matumizi ya fedha hizo, ilhali yeye kama mhasibu hatambui fedha hizo zimetumika vipi, huku Mwenyekiti (Eliya Mjata) na Katibu wa chama (Mbarouk Twiza), wakiwa hawana majibu ya kuridhisha kwa wajumbe.
“Tofauti na ujumbe, wanachama wamenichagua kama mweka hazina wao, kwa hiyo kama hela inatoka ni lazima mimi nitambue na niweke maandishi hela imefanya nini, lakini cha ajabu mweka hazina mimi sijui, watu wanakwenda kutoa pesa wao wenyewe wawili na watu tunaoweka saini pale tupo wanne, lakini mimi sijui na mwenzangu naye nadhani hajui, hata kamati kuu yenyewe haipo vizuri, kwa hiyo fedha zinapokwenda kubebwa zinabebwa na mwenyekiti na katibu tu, hela zinatoka tu na kilichofanyika hakuna.
“Mimi siku hiyo nilizuka kwenye kundi letu nikahoji hela zimefanyia nini ili tuijadili pesa ya PPF au la tuitishe kikao ije ‘bank statement’ tujadili tunafanyia kazi gani hiyo fedha kama ipo, kumbe hela wameshakula, sisi tumebakiza mwaka mmoja mwakani tunapisha watu wengine, hivi watu wengine wakienda kwenye mifuko ya jamii watasaidiwa? Mimi si ndiyo mweka saini, nikajitoa nikaenda benki kuangalia imebaki elfu 20 na ngapi sijui, pesa yote wamemaliza na mbaya hatukutaarifiwa kuwa hela imetoka.
“Hili suala nimelifikisha mpaka kwa Simon Mwakifwamba (Rais wa TAFF), kwa hiyo TAFF wanalifahamu hili na waliwaita wakaanza kutoa longolongo, we unaitwa na mabosi zako unashindwa kwenda? Kwanini wanakwepa kama hawana matatizo, halafu tena wanaanza kutuita tena tujadili mipango na matumizi ya pesa gani,” alisema Lydia.
Papaso la Burudani lilimtafuta Mwenyekiti wa Chama cha Waigizaji Tanzania, Eliya Mjata, kujibu tuhuma hizo, ambapo alimwelekeza mwandishi amtafute Katibu wake, Mbarouk Twiza, ambaye alifafanua namna fedha hiyo ilivyotumika.
“Tulipewa fedha na PPF kwa ajili ya kuandaa kongamano lililotakiwa kufanyika Machi 25 na baadaye likasogezwa mbele hadi Aprili 17, mwaka huu, kutokana na sababu zilizo nje ya uwezo wetu, lazima lifanyike kwa uwepo wa pande zote mbili na sasa tumepanga kulifanya Oktoba 14 mwaka huu, tunasubiri majibu ya PPF, kimsingi fedha zimefanya kazi iliyokusudia na tukio limegharimu zaidi ya milioni 5 katika maandalizi yake.
“Wenye wasiwasi na matumizi ya chama wanajua taratibu za kufuata ili madai yao yawe na nguvu na siyo kwenda kwenye vyombo vya habari, au mitandao ya kijamii kwa lengo la kuipotosha jamii na kuchafua majina ya watu,” alisema Twiza.
Naye Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Waigizaji Taifa, Jimmy Mafufu, alipotafutwa na BINGWA alisema muda wa kuliongelea hilo suala bado haujafika mpaka bodi itakapokaa na kutoa maelezo yatakayoazimiwa na kikao.